Habari Mpya

Wednesday, February 12, 2014

Kwa Bunge hili la Katiba, CCM wameshapiga bao

Mchakato wa Mabadiliko ya Katiba umeingia katika sura mpya ambapo uteuzi wa wajumbe 201 wa Bunge la Katiba umekamilika.
Uteuzi huo unatawaliwa na Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, Sura, 83 ambayo inaweka mamlaka ya uteuzi, masharti, taratibu, vigezo na mambo mengine yote yanayopaswa kuzingatiwa katika uteuzi wa wajumbe wa Bunge la Katiba.
Sheria hiyo inataja aina tatu za wajumbe wa Bunge la Katiba kuwa ni wabunge wote wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, wajumbe wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar na wajumbe 201 kwa mujibu wa Kifungu Na. 22(1c) cha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ambayo inaonyesha makundi mbalimbali 10 yanayohusika.
Makundi hayo ni pamoja na taasisi zisizokuwa za kiserikali (20), taasisi za kidini (20), vyama vyote vya siasa vyenye usajili wa kudumu (42) na taasisi za elimu (20).
Pia sheria inataka wateuliwe watu wenye ulemavu (20), vyama vya wafanyakazi (19, vyama vinavyowakilisha wafugaji (10), vyama vinavyowakilisha wavuvi (10), vyama vya wakulima (20) na vikundi vya watu wenye malengo yanayofanana (20).
Kutokana na sheria na muundo wa Bunge la Katiba, Chama Cha Mapinduzi (CCM) chenye wabunge wapatao 260 katika Bunge la Jamhuri ya Muungano, kimeongezewa tena kwenye makundi yaliyotajwa hapo juu, huku taasisi nyingine ambazo zilituma majina yake hata hazikufikiriwa.
Ni kweli kwamba kulikuwa na majina zaidi ya 5,000 yaliyotumwa kwenye Ofisi ya Rais. Lakini kulikuwa na sababu gani ya kuilimbikizia CCM majina zaidi wakati tayari ina wabunge wengi, na kuyaacha makundi mengine yasiyo na harufu hata ya bungeni?
Kulikuwa na ulazima gani wa rais kuteua wajumbe? Kama nafasi zilikuwa 201, kwa nini taasisi zisingeambiwa mapema zilete wajumbe kulingana na nafasi hiyo? Labda kazi ya rais ingekuwa ni kuthibitisha tu majina, lakini siyo kuwateulia watu wajumbe wasiowajua kabisa. 
Chukua mfano wa taasisi zisizokuwa za kiserikali zenye wajumbe 20. Ukiiangalia orodha ile kwa hesabu ya haraka utaona kuna makada waaminifu wa CCM watano na hilo ni kundi moja tu. Walau kila kundi kuna makada watiifu wa CCM.
Kwa jumla CCM watakuwa na zaidi ya asilimia 70 ya wajumbe wa Bunge la Katiba. Je, makundi ya watu wasio na sauti yatasikilizwa? Hiyo Katiba itakuwa ya wananchi au ya chama tawala?
Sijagusia vyama vya siasa ambavyo walau vimekumbukwa kwa kupewa wajumbe wawili watatu. Lakini hawatafua dafu mbele ya CCM.
Kumbuka kuwa, CCM haikuwa na hata wazo la kuandika Katiba. Walidaka tu hoja za vyama vya upinzani na wanaharakati. 
Hivi sasa ndiyo wamekamata usukani. Kama hawataki serikali tatu, basi wameshinda, kama wanataka kusimika utawala wao milele, hakuna wa kuwazuia. Kidumu Chama cha Mapinduzi.

Na Elias Msuya,Mwananchi
  • Blogger Comments
  • Facebook Comments

0 comments:

Item Reviewed: Kwa Bunge hili la Katiba, CCM wameshapiga bao Description: Rating: 5 Reviewed By: mcjohnminja.blogspot.com
Scroll to Top