Habari Mpya

Tuesday, March 08, 2016

Sawa... MMEACHANA, KUNUNIANA NDIYO DAWA?

NAMSHUKURU Mungu kwa kunikutanisha na wewe tena msomaji wa safu hii ya Love Story. Huu ndiyo uwanja wetu wa kuweza kupeana mambo mbalimbali ambayo yanatu zunguka katika ulimwengu wa uhusiano.
 
Ni ukweli usiopingika kwamba, mtu anapoanzisha uhusiano, akadumu, siku zote hatarajii kama kuna siku penzi linaweza kuvunjika. ‘Anainjoi’ utamu wa mapenzi. Anapenda jinsi mwenzake anavyomjali na kumuona wa thamani kuliko kitu kingine.
 
Akili na mawazo yake yote huwa yanakuwa kwa mpenzi wake. Kuna wakati anapitiliza kupenda utafikiri kachanganyikiwa kumbe wapi, ni mapenzi tu ndio yanampeleka puta. Anampenda mwenzake kiasi cha kuona kama wamekuwa ndugu wa tumbo moja.
Ukaribu na mpenzi wake unamfanya ajisahau kabisa. Anafurahishwa na ucheshi wake, utundu wake na kila kitu kinachagiza mapenzi. Dunia yote anaiona kama ni yake na mpenzi wake. Wengine wote wasindikizaji tu. Hayo ndiyo mapenzi!
 
Ukifika wakati penzi likayumba, likafa ghafla, mara nyinyi ambaye hakuwa amejiandaa hupata maumivu makali ya moyo. Anapata maumivu kwa sababu anakuwa hajajiandaa kisaikolojia. Akili yake iliamini watadumu milele. Bahati mbaya mwenzake kwa wakati huo haumii sana kwa sababu yeye alishajiandaa na pengine alikuwa hana lengo la kufika mbali na mwenzake, alikuwa akimchezea tu.
 
Kwa yule ambaye hakujiandaa anateseka. Anakumbuka ukaribu aliokuwa ameuweka kwa mwenzake. Namna ambavyo wamekuwa wakila, wakitoka ‘out’ pamoja na kufanya starehe mbalimbali za kusherehesha penzi ndivyo vitu vinavyompa mawazo.
Anajiuliza kwamba ‘vurugu’ zote zile ndio zimefika ukingoni. Kwamba kwa nini mwenzake hakumuweka wazi tangu mwanzoni kwamba hampendi ili ajue moja?
 

Anawaza kumzoea kote mwenzake ndio kumefikia mwisho? Haamini. Hataki kukubaliana na matokeo. Anamuona mwenzake kama adui.
Hata kama mwenzake atamueleza kistaarabu. Kwamba kutokana na sababu zilizo nje ya uwezo wake, haiwezekani kuendelea na safari. Bado inakuwa ngumu kukubaliana na ukweli huo.

Kipindi hicho, ndicho cha kununiana. Aliyetendwa anaamua kumnunia mwenzake akiamini labda ndio dawa ya kumpunguzia machungu.
Hataki kabisa kumuona mwenzake. Anamnunia ileile. Anafika wakati hadi marafiki wa aliyekuwa mpenzi wake nao anawanunia. Wote wanakuwa maadui, anaamini wote lao moja. Kumbe pengine maskini ya Mungu, hawahusiki kwa lolote.
Ndugu zangu, mapenzi siyo vita. Japo kweli penzi linapofikia kikomo ambaye hakujiandaa siku zote huwa ni vigumu kukubaliana na matokeo lakini tunapaswa kujifunza kufanya maamuzi ya busara.

Hakuna haja ya kununiana. Unavyoumia wewe, hata yeye anaweza kuumia pia. Kukuacha hujui amekuepusha na nini. Pengine haikupangwa muendelee na urafiki au kuwa wanandoa.
 
 Ni vizuri ukamuweka mbali mtu mliyeachana lakini ikitokea mmekutana, msalimiane.
Haikupunguzii kitu. Penzi linakuwa limeisha lakini ubinadamu unabaki palepale.Kwa kipindi fulani, jaribu kukaa mbali na yule mliyeachana. Haimaanishi umnunie, pata muda mwingi sana wa kufanya mambo yako. Jishughulishe na vitu ambavyo vitakuondoa kabisa katika suala la kuwaza mapenzi.
 
Usikurupuke kuanzisha uhusiano mpya kwani ni hatari sana kwa wakati huo. Unaweza kuanzisha na mtu ambaye hana sifa nzuri na ukajikuta unaambulia maumivu kwa mara nyingine.Baada ya muda fulani utazoea, aliyekuacha mnaweza kuzungumza vizuri. Mkawa mnawasiliana kama kawaida japo kwa wakati huo suala la mapenzi litakuwa halipo.
 
Mtakie kila la kheri katika safari yake kama kweli mtakuwa mmefikia hatua ya kutorudi nyuma. Yawezekana mwenzako alifanya maamuzi yale kwa kukurupuka, akajishusha na mkaendelea na safari kama kawaida.

Hakuna sababu ya kumnunia mtu ambaye mlikuwa kitu kimoja. Mlishirikiana na mambo mengi. Anakujua na wewe unamjua vizuri. Zidhibiti hasira. Hata kama alikosea kiasi gani, mfanye rafiki na maisha yaendelee.
 
Ikitokea amepata mchumba mwingine akakuambia, mtakie kila la kheri na hata wewe utakapompata wako, hana budi kukuunga mkono na mkawa watu wa kuwasiliana kama watu mliowahi kusindikiza safari ya maisha pamoja.
  • Blogger Comments
  • Facebook Comments

0 comments:

Item Reviewed: Sawa... MMEACHANA, KUNUNIANA NDIYO DAWA? Description: Rating: 5 Reviewed By: mcjohnminja.blogspot.com
Scroll to Top